Showing posts with label magonjwa ya mifugo. Show all posts
Showing posts with label magonjwa ya mifugo. Show all posts

Tanzania yazindua kampeni ya Chanjo ya Mifugo na UtambuziAfyaclass Forum •

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeanza utekelezaji wa kampeni ya kitaifa ya Chanjo na Utambuzi wa Mifugo Wilayani Longido ambapo takribani mifugo 2000 imechanjwa.



Tukio hilo lililoongozwa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji Julai 02, 2025 limefanyika ikiwa ni takribani wiki mbili baada ya Uzinduzi wa kampeni hiyo uliofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu.

Akizungumza wakati wa utekelezaji wa kampeni hiyo Mhe. Dkt. Kijaji amewataka wafugaji wote nchini kutumia fursa hiyo iliyotolewa na Rais Samia kupitia ruzuku ya nusu bei kwa upande wa Ng’ombe, Mbuzi na Kondoo na chanjo ya bila gharama yoyote kwa upande wa kuku wa kienyeji.

“Naomba wataalam wote wa Mifugo tusikae ofisini twendeni uwandani tukatatue changamoto zote za wafugaji” Ameongeza Mhe.Dkt. Kijaji.

Aidha Dkt. Kijaji ameongeza kuwa Serikali imeamua kuendesha kampeni hiyo ili kuiwezesha nchi kuuza mifugo na mazao yake kwenye masoko ya nje ambayo awali yalishindwa kupokea kutokana na changamoto ya kutokuwa na ithibati ya Usalama wa Mifugo na Mazao yake ambapo amebainisha kuwa tayari nchi za Misri na Falme za kiarabu zipo tayari kuanza kununua mifugo hai kutokana na jitihada hizo.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Kenan Kihongosi amemhakikishia Dkt. Kijaji kuwa wafugaji wa mkoa huo wapo tayari kuchanja mifugo yao na kutambua kupitia hereni za kielektroniki huku pia akiwataka wafugaji kuendelea kufuga kisasa ili kuinua uchumi wa mkoa huo ambao idadi kubwa ya wananchi wake ni Wafugaji.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wafugaji Wilayani Longido Bw. Joseph Sadera ameishukuru Serikali kwa kuwapatia ruzuku kwenye chanjo hizo ambapo ameongeza kuwa jambo hilo limewaongezea chachu ya kufuga kisasa na kuboresha maisha yao kupitia masoko ya mifugo na mazao yake watakayopata baada ya kuchanja mifugo yao.

Mhe. Dkt. Kijaji anatarajiwa kuendelea kukagua utekelezaji wa zoezi hilo katika mikoa ya Mara, Simiyu,Tabora, Geita, Pwani, Morogoro na Dodoma.

0 Comment

Tahadhari wanaotumia ARVs kunenepesha mifugoAfyaclass Forum •

Tahadhari wanaotumia ARVs kunenepesha mifugo 

Serikali na Mamlaka ya Dawa na Vifaatiba Tanzania (TMDA) zimetoa tahadhari ya matumizi  ya dawa za kufubaza makali ya virusi vya Ukimwi (ARVs) kunenepesha mifugo, ikitajwa kuwa ni athari kwa afya ya jamii.

Mbali na usugu unaosababishwa na ARV, utafiti uliofanyika mwaka 2018 ulionyesha kuwa asilimia 90 ya wafugaji wanatumia dawa za antibiotiki kutibu wanyama badala ya chanjo.

TMDA imetoa onyo hilo Jana Jumapili, Septemba 22, 2024 ikiwa ni siku mbili tangu wanasayansi, watafiti kukutana kujadili, matumizi holela ya ARV yanavyochangia usugu wa dawa hizo.

Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa TMDA, Adam Fimbo imeeleza kuwa mamlaka imepata taarifa juu ya uwepo wa baadhi ya wafugaji wanaotumia vibaya dawa hizo kwa lengo la kunenepesha mifugo yao, akikemea matumizi hayo kwa kuwa yana madhara kwa afya ya jamii.

Kwa upande wake,  Mfamasia Mkuu wa Serikali, Daudi Msasi amesema kitendo hicho ni kinyume cha sheria za nchi na suala hilo linaanza kufuatiliwa na Wizara ya Afya na Wizara ya Mifugo na uvuvi kwa pamoja.

“Serikali haikubaliani na hili, yeyote anayefanya hivyo anakiuka kanuni na taratibu, kwa hiyo TMDA wanafuatilia ili kujua nani anafanya na hatua za kisheria zitafuata kwa watakaobainika,” amesema Msasi.

Via;Mwananchi

0 Comment

Kuna zaidi ya magonjwa 200 yanayohusishwa na wanyama kuhamia kwa binadamuAfyaclass Forum •

Kuna zaidi ya magonjwa 200 yanayohusishwa na wanyama kuhamia kwa binadamu

Wataalamu wa mifugo wakiwa katika ufunguzi wa mafunzo ya miezi minne  yaliyoratibiwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) kwa ufadhili wa Shirika la Misaada la Marekani (USAID), yenye lengo la kuwezesha wataalamu wa mifugo kubaini, kuzuia na kurekodi magonjwa ya wanyama yaambukizwayo kwa binadamu, Jijini Dar es Salaam.

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Profesa Riziki Shemdoe amewataka wataalamu wa mifugo nchini kuwa mstari wa mbele kuzuia usambazaji wa magonjwa ya mifugo kushambulia binadamu ili kuisaidia Serikali kutotumia fedha nyingi kutibu magonjwa yanayozuilika.

Amesema kuzuia magonjwa ya wanyama kwenda kwa binadamu ni rahisi kuliko matibabu ambayo huhitaji fedha na muda mwingi.

Profesa Shemdoe ameyasema hayo leo Septemba 19,2024 jijini Dar es Salaam wakati akifunga mafunzo ya miezi minne yaliyoratibiwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) kwa ufadhili wa Shirika la Misaada la Marekani (USAID) yakilenga kuwezesha wataalamu wa mifugo kubaini, kuzuia na kurekodi magonjwa ya wanyama yaambukizwayo kwa binadamu.

"Mafunzo haya ni muhimu sana kwa wataalamu wa mifugo, kutibu magonjwa ya mifugo kwa binadamu tunatumia fedha nyingi kuliko kuyaangalia magonjwa haya mapema.

“Ni muhimu kuwa mstari wa mbele kuzuia magonjwa haya kwenda kwa binadamu kufanya hivyo tutakuwa tumesaidia kuokoa fedha nyingi za Serikali ambazo zingetumika kwenye matibabu," amesema.

Hoja hiyo inafafanuliwa na Mratibu wa Mafunzo ya Epidemiolojia na Usimamizi wa Maabara wa Wizara ya Afya Dk Rogath Kishimba akisema, chanjo ya mifugo gharama yake ni ndogo lakini ugonjwa ukihamia kwa binadamu kutoka kwa mnyama gharama ya matibabu ni kubwa.

Akitolea mfano wa kichaa cha mbwa, Dk Kishimba amesema chanjo hiyo huchanjwa mbwa kwa Sh2,000 lakini mtu anapong'atwa na mbwa mwenye ugonjwa huo hulazimika kupata chanjo nne ambazo hutolewa kwa Sh30,000 hadi Sh60,000 kwa dozi moja.

Profesa Mdoe amewataka wataalamu hao kutumia mafunzo waliyopata kuchanja mifugo ili Tanzania iendelee kukuza soko la nyama kimataifa, kwani tayari kuna nchi inaangalia uwezekano wa kuagiza tani 54,000 za nyama kutoka nchini.

Kwa upande wake Dk Kishimba amesema mtu anapopatwa na kichaa cha mbwa na kuanza kuonyesha dalili, uwezekano wa kupona kwake ni mdogo.

"Ukiwa na wagonjwa 100 ni wastani wa wagonjwa wawili pekee ndio wanaweza kupona au wote wasipone kabisa, ndio maana tunasisitiza muhimu kuadhibiti, yakiwa kwa wanyama ni nafuu kutibu na kuzuia," amesema.

Naye, Mkurugenzi wa huduma za mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dk Benezeth Lutege amesema katika kuongeza upatikanaji bora wa chanjo, Serikali imeondoa kodi ya chanjo za mifugo zinazoingizwa kutoka nje ya nchi.

"Chanjo na dawa za mifugo nchini zinaingizwa bila kodi, kwahiyo gharama za chanjo tunategemea zitakuwa ndogo. Pia, tuna chanjo ya mbwa tunatarajia kuzalisha na ipo katika hatua mbalimbali za uzalishaji na huenda hadi 2030 tutakuwa tumeanza kuzalisha, pia tumeandaa mkakati wa kutokomeza kichaa cha mbwa 2024 hadi 2028 na tumeshawasilisha Shirika la Nyama Duniani," amesema.

Mkakati huo utakapopitishwa utaipa Tanzania nafasi ya kuanza kupokea chanjo ya kichaa cha mbwa kutoka kwenye shirika hilo.

Kwa hali ilivyo, mtaalamu wa mifugo kutoka Masasi Innocent Mrope amesema katika watu 300 walio na umri wa miaka 18 na kuendelea waliowafanyia utafiti katika vijiji 15 wilayani hapo, asilimia 54.6 hawana uelewa kuhusu kichaa cha mbwa na asilimia 32.3 walikuwa na mtazamo hasi kuhusu tatizo hilo.

Amesema ni muhimu wilaya hiyo ikajikita kutoa elimu kwa wananchi kuhusu kichaa cha mbwa kwani asilimia 14 pekee ndio wenye mtazamo chanya kuhusu ugonjwa huo, wengi wao wanapopata tatizo linalohusisna na ugonjwa huo hawaamini kupona kupitia matibabu au kuchanja mbwa wao.

Akizungumzia wahitimu wa mafunzo hayo, Mratibu wa Programu FAO Mosses Ole Neselle amesema wataalamu wa mifugo waliowezeshwa mafunzo hayo ni 30 kutoka Tanzania bara 20 na Zanzibar 10.

Amesema mafunzo hayo ni muhimu kwasababu magonjwa ya wanyama yanahatarisha usalama wa chakula duniani na kuzorotesha uchumi wa nchi.

Wataalamu waliojengewa uwezo wanaweza kukusanya taarifa, kufanya utafiti wa magonjwa ya mlipuko na kubaini viashiria vya magonjwa.

Takwimu zilivyo

Kwa mujibu wa Taasisi ya Magonjwa ya Wanyama Duniani asilimia zaidi ya 70 ya magonjwa yanayotokea duniani ni kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu.

Magonjwa yanayoambukizwa binadamu yatokayo kwa wanyama ni mafua ya ndege, kichaa cha mbwa, marburg ugonjwa wa Ebola na MPox.

Kuna zaidi ya magonjwa 200 yanayohusishwa na wanyama kuhamia kwa binadamu, hii ikiwa na maana kwamba  magonjwa 6 kati ya 10 ya kuambukiza ambayo huathiri watu husambazwa na wanyama, ikiwa ni pamoja na wanyama wafugwao nyumbani hiyo ni kwa mujibu wa Kituo cha Marekani cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (CDC).

Tovuti ya National Library of Medicine ya nchini Marekani inaonyesha magonjwa yahamayo kwa wanyama kwenda kwa binadamu, yameripotiwa matukio bilioni 2.5 vifo milioni 2.7 vikishuhudiwa.

Via,Mwananchi.

0 Comment

Ugonjwa wa Kimeta,chanzo,dalili na Tiba(Anthrax)Afyaclass Forum •

 Ugonjwa wa Kimeta,chanzo,dalili na Tiba(Anthrax)

Ugonjwa wa Kimeta(Anthrax)

Ugonjwa wa Kimeta au Anthrax ni ugonjwa unaosababiswa na bacteria wanaojulikana kama Bacillus anthracis.

Ugonjwa huu wa kimeta unaweza kuathiri binadamu na wanyama,wanyama hao wanaweza kuwa wa porini au mifugo kama vile;

  • ng'ombe,
  • nguruwe,
  • ngamia,
  • kondoo,
  • mbuzi, nk.

Pia fahamu kwamba, Bakteria hawa wanaosababisha ugonjwa wa kimeta ambayo hupatikana kama spores, wanaweza kupatikana kwenye udongo, pamba, au nywele za wanyama walioambukizwa.

Ugonjwa wa Kimeta au Anthrax huweza kumuathiri binadamu kwa njia kubwa tatu(3);

  1. Kwa njia ya maambukizi ya ngozi(Skin infection), kwa kugusana moja kwa moja na wanyama walioambukizwa kupitia majeraha,vidonda au sehemu ya ngozi ulipokatwa
  2. Kupitia kula nyama mbichi au ambayo haijaiva vizuri kutoka kwa wanyama walioambukizwa au kupitia kunywa maziwa yao.
  3. Kuvuta pumzi yaani Inhalation, ambapo unavuta hewa ndani pamoja na Spores za bacteria wanaosababisha ugonjwa wa kimeta (Hii ni aina mbaya zaidi ya ugonjwa huu)

Maambukizi haya ya Ugonjwa wa kimeta kwa njia ya ngozi(Skin infection) kawaida ni maambukizi ya ngozi, ambapo watu huambukizwa kwa kushika wanyama au bidhaa za wanyama ambazo zina spores,

Hii mara nyingi hutokea kwa madaktari wa mifugo, wafanyakazi wa kilimo, wazalishaji wa mifugo au wachinjaji wanaoshughulika na wanyama wagonjwa, au wakati maambukizi yameenezwa na pamba au ngozi.

Dalili za Ugonjwa wa Kimeta

1. Kwa wanyama, Ugonjwa wa kimeta huweza kusababisha dalili kama vile;

  • homa kali,
  • udhaifu au kudhoofika kwa mnyama,
  • kukosa hamu ya kula,
  • kutokwa na damu kwenye matundu yote ya mwili (pua, mdomo, masikio, njia ya haja kubwa n.k.),
  • kupata shida ya kupumua
  • Pamoja na kuharisha damu.
  • Pia Ugonjwa wa kimeta unaweza kusababisha kifo cha ghafla.
  • Damu ya mnyama aliyeambukizwa kimeta HAIGANDI wakati wa kuchinja. Pia, wakati wa kuchinja, kuna uvimbe wenye alama na kuoza kwa haraka.

2. Kwa wanadamu, kulingana na aina (ilivyoelezwa hapo juu) na njia ya maambukizi, Ugonjwa wa kimeta(anthrax) kwa binadamu unaweza kusababisha dalili kama vile;

  • Kupata homa,
  • vidonda vya ngozi visivyo na maumivu
  • Kuwa na alama nyeusi inayoonekana baada ya malengelenge,
  • Mwili kukosa nguvu au kuwa na udhaifu wa jumla wa mwili,
  • Kupata shida ya kupumua.
  • Pia ugonjwa wa kimeta unaweza kusababisha ugonjwa mkali kwenye mfumo wa umeng'enyaji chakula(digestive illness) unaofanana na sumu kwenye chakula(food poisoning).

Nani yupo kwenye hatari ya Kupata Ugonjwa wa kimeta?

Watu hawa wapo kwenye hatari zaidi ya kupata Ugonjwa wa kimeta;

1. Watu wanaoshughulikia wanyama, yaani,

  • madaktari wa mifugo,
  • wafanyakazi wa maabara ya mifugo,
  • wakulima,
  • wafanyakazi wa machinjio,
  • wachinjaji,
  • wafugaji wa ng'ombe,
  • wazalishaji na wafanyabiashara wa mifugo,
  • watunza wanyamapori,
  • wawindaji,
  • walinzi wa mbuga,
  • wasindikaji,
  • waagizaji na wasafirishaji wa ngozi,
  • wahudumu wa afya ya wanyama. na kadhalika.

2. Watu wanaokula wanyama (ng'ombe, kondoo, na mbuzi) waliopatikana wamekufa

3. Wafanyakazi wa afya,

4. wafanyakazi wa maabara ya uchunguzi

5. watoa huduma ambao wanahudumia vidonda vya mgonjwa aliyeambukizwa

6. Maafisa wa kutekeleza sheria (Polisi, Jeshi, Uhamiaji, Forodha, pamoja na Wafanyikazi wengine.)

7. Yeyote anayesafiri hadi eneo ambapo kuna kisa kilichothibitishwa cha ugonjwa wa kimeta.

0 Comment
Notification
My blog is in the process of editing and perfecting the new template, so there are still some functions to click but not yet used. Note which blogs associated with your side please read this lesson to update the blog logo.
UNDERSTOOD