FIFA Yafanya Mazungumzo na Iran Kuhusu Ushiriki wa Kombe la Dunia 2026 Marekani
Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu duniani, FIFA limeeleza kuwa lina matumaini makubwa kwamba timu ya taifa ya Iran itashiriki kikamilifu katika Kombe la Dunia la mwaka 2026 licha ya mvutano wa kisiasa unaoendelea kati ya Iran, Israel na Marekani.
Katibu Mkuu wa FIFA, Mattias Grafstrom alitoa kauli hiyo baada ya kufanya kikao na rais wa Shirikisho la Soka la Iran, Mehdi Taj mjini Istanbul siku ya Jumamosi Mei 16.
Grafstrom alisema mazungumzo hayo yalikuwa mazuri na yenye kujenga ushirikiano, akisisitiza kuwa FIFA inaendelea kufanya kazi kwa karibu na Iran kuhakikisha taifa hilo linakaribishwa kwenye mashindano hayo makubwa ya dunia.
Kombe la Dunia la mwaka 2026 litafanyika kuanzia Juni 11 hadi Julai 19 katika mataifa ya Marekani, Canada na Mexico. Iran imepangwa kucheza mechi zake zote za Kundi G nchini Marekani, jambo ambalo limezua wasiwasi kutokana na hali ya kisiasa iliyopo.
Wasiwasi huo uliongezeka baada ya baadhi ya maafisa wa soka wa Iran kuzuiwa kuingia Canada kuhudhuria mkutano wa FIFA uliofanyika mjini Vancouver. Ujumbe wa Iran ulioongozwa na Taj ulirudishwa katika uwanja wa ndege wa Toronto licha ya kuwa na visa halali.
Taarifa zinaeleza kuwa mamlaka za Canada zilihusisha tukio hilo na madai ya uhusiano wa baadhi ya viongozi hao na kikosi cha Islamic Revolutionary Guard Corps ambacho Canada ilikiweka katika orodha ya makundi ya kigaidi mwaka 2024.
Hata hivyo, FIFA imeeleza kuwa tayari imejadili masuala yote muhimu yanayohusiana na visa pamoja na maandalizi ya usafiri kwa wachezaji na viongozi wa Iran kuelekea mashindanoni.
Kwa upande wake, Taj alisema FIFA ilisikiliza hoja zote 10 zilizowasilishwa na Shirikisho la Soka la Iran na kutoa majibu pamoja na suluhisho kwa kila hoja.
Iran hapo awali iliomba baadhi ya mechi zake zihamishiwe nchini Mexico kutokana na hofu ya kucheza Marekani, lakini Rais wa FIFA Gianni Infantino alisisitiza kuwa ratiba na viwanja vitabaki kama vilivyopangwa.
Timu ya taifa ya Iran maarufu kama Team Melli inatarajiwa kuweka kambi nchini Türkiye kabla ya kuelekea Tucson nchini Marekani kwa maandalizi ya mwisho ya mashindano hayo.
Iran itaanza kampeni yake ya Kombe la Dunia kwa kucheza dhidi ya New Zealand mjini Los Angeles Juni 15 kabla ya kukutana na Belgium na Egypt katika michezo mingine ya Kundi G.
Wakati huohuo, kocha wa Iran Amir Ghalenoei ametetea uteuzi wa kikosi chake cha awali cha wachezaji 30 baada ya mshambuliaji nyota Sardar Azmoun kuachwa nje ya kikosi hicho.
Azmoun ambaye aliwahi kuonyesha kuunga mkono maandamano dhidi ya serikali ya Iran, hivi karibuni alikosolewa na vyombo vya habari vya serikali baada ya kuonekana kwenye picha akiwa pamoja na Emir wa Dubai.
Kocha Ghalenoei amesema uteuzi wa kikosi hicho ulizingatia uwezo wa kiufundi pekee na haukuathiriwa na masuala ya kisiasa.
Iran sasa imefanikiwa kufuzu Kombe la Dunia kwa mara ya nne mfululizo, jambo linaloonyesha maendeleo makubwa ya soka la taifa hilo katika miaka ya hivi karibuni.

.jpeg)



Post a Comment
Related Discussions...