Timu ya Iran ya Kombe la Dunia Bado Yasubiri Visa za Marekani, Balozi Asema
Timu ya taifa ya Iran bado haijapatiwa visa za kuingia Marekani kuelekea mashindano ya Kombe la Dunia 2026, jambo ambalo limeibua wasiwasi mkubwa kuhusu maandalizi yao kabla ya kuanza kwa michuano hiyo.
Balozi wa Iran nchini Mexico, Abolfazl Pasandideh, amesema timu hiyo haishiriki mashindano katika mazingira ya usawa kutokana na changamoto za kupata visa pamoja na matatizo ya kufanya mazoezi kwa utulivu kabla ya mechi zao za kundi.
Balozi huyo alizungumza akiwa katika mji wa Tijuana uliopo mpakani mwa Mexico na Marekani, ambako timu ya Iran imehamishia kambi yake ya mazoezi. Awali, timu hiyo ilikuwa imepanga kuweka kambi mjini Tucson, Arizona nchini Marekani, lakini mipango hiyo ilibadilika kutokana na kuchelewa kwa vibali vya kuingia nchini humo.
Akizungumza na waandishi wa habari, Pasandideh alisema Marekani haijatimiza wajibu wake kama mwenyeji wa mashindano hayo kwa kushindwa kuhakikisha timu hiyo inapatiwa visa kwa wakati.
“Bado hatujui kama wachezaji watapatiwa visa zao au la,” alisema balozi huyo.
Iran inatarajiwa kucheza mechi zake zote za hatua ya makundi nchini Marekani, ambapo itaanza kwa kucheza dhidi ya New Zealand mjini Los Angeles tarehe 15 Juni, kabla ya kukutana na Belgium tarehe 21 Juni, na baadaye kucheza dhidi ya Egypt mjini Seattle tarehe 26 Juni.
Shirikisho la Soka la Iran pia limethibitisha kuwa lilikuwa linaomba wachezaji wake kupewa visa vya kuingia mara nyingi ili kurahisisha safari zao wakati wa mashindano hayo.
Pasandideh amesema vita vinavyoendelea Mashariki ya Kati tangu Februari 28 pia vimeathiri vibaya maandalizi ya timu hiyo, hali iliyofanya washindwe kufanya mazoezi kwa utaratibu unaostahili.
Katika hatua nyingine, Marekani, Mexico na Canada zimetangaza hatua za pamoja za kiafya kwa wasafiri wanaotoka maeneo yenye hatari kubwa ya Ebola barani Afrika, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya usalama kuelekea Kombe la Dunia 2026.
Nchi hizo zilisema afya na usalama wa wananchi pamoja na wageni wanaotarajiwa kuhudhuria mashindano hayo ni kipaumbele kikubwa wakati huu ambao dunia inaendelea kufuatilia mlipuko wa Ebola katika baadhi ya maeneo ya Afrika.
Shirika la Afya Duniani (WHO) lilitangaza rasmi tarehe 17 Mei kwamba mlipuko wa Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ni dharura ya afya ya kimataifa kutokana na hofu ya kusambaa kwa ugonjwa huo katika mataifa jirani.




Post a Comment