Head

Jeshi la Marekani limeanzisha mashambulizi mapya dhidi ya Iran huku

Jeshi la Marekani limeanzisha mashambulizi mapya dhidi ya malengo ya kijeshi ndani ya Iran huku mvutano kati ya mataifa hayo mawili ukiendelea kuongezeka. Hatua hiyo imekuja baada ya Rais wa Marekani, Donald Trump, kuonya kuwa Tehran itakabiliwa na mashambulizi makali zaidi iwapo juhudi za kidiplomasia zitashindwa kufanikisha makubaliano ya amani.

Kwa mujibu wa Kamandi Kuu ya Jeshi la Marekani (CENTCOM), vikosi vya Marekani vilifanya mashambulizi ya kujilinda kwa kutumia ndege za kivita pamoja na silaha za kisasa zinazolenga shabaha kwa usahihi mkubwa. Mashambulizi hayo yalielekezwa kwenye mifumo ya mawasiliano ya kijeshi na maeneo ya ulinzi wa anga katika sehemu mbalimbali za Iran.

CENTCOM ilisema operesheni hiyo ilihusisha vikosi vya Jeshi la Wanamaji, Jeshi la Anga pamoja na vikosi vya majini vya Marekani, vikilenga maeneo yaliyotajwa kuwa tishio kwa wanajeshi wa Marekani na meli za biashara zinazopita katika eneo la Ghuba ya Uajemi na Mlango wa Hormuz.

Katika taarifa yake, CENTCOM ilieleza kuwa hatua hiyo ni jibu la moja kwa moja kwa kile ilichokiita vitendo vya uchokozi vinavyoendelea kutoka upande wa Iran. Kamandi hiyo pia ilisisitiza kuwa vikosi vya Marekani vipo katika hali ya tahadhari ya juu na viko tayari kujibu mashambulizi yoyote zaidi yatakayoweza kutokea.

Awali, jeshi hilo lilitangaza kuwa mashambulizi hayo yalianza majira ya usiku kwa saa za Mashariki ya Kati, yakilenga malengo kadhaa ya kijeshi ndani ya Iran.

Akizungumza katika Ikulu ya White House, Trump alisema Marekani itaendelea na operesheni zake za kijeshi huku ikiendeleza juhudi za kutafuta suluhisho la kidiplomasia.

“Tutakuwa tukiwashambulia kwa nguvu sana,” alisema Trump alipokuwa akizungumzia tukio la kudunguliwa kwa helikopta ya Marekani aina ya Apache katika Mlango wa Hormuz.

Pamoja na msimamo huo mkali, Trump alisema Marekani bado inaamini katika uwezekano wa kufikia makubaliano mapya na Tehran kuhusu mpango wake wa nyuklia.

“Tunataka makubaliano yenye maana na yanayoweza kufanya kazi,” alisema rais huyo, akiongeza kuwa Iran tayari imeonyesha utayari wa kutotengeneza silaha za nyuklia ingawa makubaliano rasmi bado hayajakamilika.

Trump pia alidai kuwa Marekani imekuwa ikizuia kwa siri usafirishaji wa mafuta kutoka Iran, hatua ambayo alisema imechangia kuzuia kupanda kwa bei ya mafuta duniani.

Kwa upande wake, Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Pete Hegseth, alisema Iran haitakuwa na busara kuendelea kuichokoza Marekani baada ya mashambulizi hayo mapya.

Akiwa katika ziara kwenye kambi ya kijeshi ya Guantanamo Bay nchini Cuba, Hegseth alisema operesheni hizo zinalenga kulinda wanajeshi na maslahi ya Marekani katika eneo hilo.

Aidha, alisisitiza kuwa utawala wa Trump bado unalenga kufanikisha makubaliano yatakayozuia kabisa Iran kumiliki silaha za nyuklia, akisema Marekani inataka makubaliano “bora na yenye uhakika” kwa usalama wa taifa hilo.

#Reply

#5Replies