Showing posts with label PEPFAR/UNAIDS. Show all posts
Showing posts with label PEPFAR/UNAIDS. Show all posts

UNAIDS inakadiria kutatokea maambukizi mapya ya VVU milioni 6 na vifo vya ziada ya milioni 4 kati ya 2025 na 2029Afyaclass Forum •

Shirika la Umoja wa Mataifa la kukabiliana na UKIMWI, UNAIDS leo limezindua ripoti yake ya mwaka huu wa 2025 ya hali ya Ugonjwa wa UKIMWI. “UKIMWI, Janga  na mabadiliko,” inayoonesha kuwa kuna janga kubwa la kifedha linalotishia kuvuruga mafanikio yaliyopatikana kwa miongo kadhaa, isipokuwa mataifa yatekeleze mabadiliko makubwa katika programu na ufadhili wa ugonjwa wa Virusi Vya Ukimwi, VVU, Imesema ripoti iliyotolewa leo na Shirika hilo la UNAIDS mjini Geneva Uswisi na Johannesburg, Afrika Kusini.



Ripoti hiyo inasisitiza athari za ghafla za upunguzaji mkubwa wa ufadhili kutoka kwa wafadhili wa kimataifa, hasa katika nchi zilizoathirika zaidi na VVU. Hata hivyo, inatoa mifano ya kuhamasisha ya nchi na jamii ambazo zimeonesha uimara kwa kuendeleza mapambano dhidi ya UKIMWI licha ya changamoto kubwa.

Kati ya nchi 60 za kipato cha chini na cha kati zilizojumuishwa katika ripoti, 25 zimeonesha nia ya kuongeza bajeti zao za ndani kwa ajili ya kukabiliana na VVU ifikapo 2026. Ongezeko hili linakadiriwa kuwa la asilimia 8, sawa na takribani dola milioni 180 za Kimarekani — hatua nzuri lakini bado haitoshi kufidia upungufu wa ufadhili wa kimataifa katika nchi zinazoitegemea pakubwa.

Janga la kimataifa: Upungufu mkubwa wa fedha watishia kurejesha nyuma mafanikio

Licha ya mafanikio yaliyoonekana katika mwaka wa 2024, kupungua kwa misaada ya kimataifa na upungufu mkubwa wa fedha katika mwaka wa 2025 umesababisha machafuko katika mifumo ya afya, kukatiza huduma za msingi za afya, na kupunguza huduma za kinga na tiba dhidi ya VVU.

Nchini Msumbiji pekee, zaidi ya wahudumu wa afya 30,000 wameathirika. Nchini Nigeria, idadi ya watu wanaoanza kutumia dawa za kuzuia maambukizi ya VVU (PREP) imeshuka kutoka watu 40,000 hadi 6,000 kwa mwezi. Ikiwa huduma zinazofadhiliwa na Marekani zitakoma kabisa, UNAIDS inakadiria kutatokea maambukizi mapya ya VVU milioni 6 na vifo vya ziada ya milioni 4 kati ya 2025 na 2029.

Mkurugenzi Mtendaji wa UNAIDS, Winnie Byanyima anasema, “Hii si pengo la kifedha tu -ni bomu linalosubiri kulipuka. Tumeona huduma zikisimama ghafla. Wahudumu wa afya wamerejeshwa nyumbani. Na watu, hasa watoto na makundi muhimu wakikosa huduma.”

Tayari kufikia 2024, watu milioni 9.2 waliokuwa wakiishi na VVU hawakuwa wakipata dawa za kuokoa maisha. Miongoni mwao, watoto 620,000 wenye umri wa miaka 0 hadi 14 hawakupata tiba, na kusababisha vifo vya watoto75,000.

Watu 630,000 walifariki dunia kutokana na UKIMWI, asilimia 61 kati yao wakiwa Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara. Wasichana balehe na wanawake vijana zaidi ya 210,000 wenye umri wa miaka 15–24 waliambukizwa ugonjwa wa VVU mwaka huo, wastani wa maambukizi mapya 570 kwa siku.

Huduma za kinga dhidi ya VVU zimevurugika pakubwa. Huduma zinazoendeshwa na jamii, ambazo ni muhimu kwa makundi ya pembezoni, zimekosa ufadhili kwa kasi ya kutisha. Mapema 2025, zaidi ya asilimia 60 ya mashirika ya wanawake yanayotoa huduma za VVU yalikuwa yamepoteza ufadhili au kulazimika kusitisha huduma zao.

Mpango wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kukabiliana na UKIMWI (PEPFAR) ulifikia wasichana na wanawake vijana milioni 2.3 wenye huduma za kina za kuzuia VVU mwaka 2024 na kuwezesha watu milioni 2.5 kutumia VVU PrEP, lakini programu hizi sasa zimeacha kabisa.

Wakati huo huo, ongezeko la sheria kandamizi dhidi ya mahusiano ya watu wa jinsia moja, utambulisho wa kijinsia, na matumizi ya dawa za kulevya limezidisha janga hili kwa kufanya huduma za VVU kutopatikana kwa watu wanaozihitaji zaidi. Nchi kama Uganda, Mali na Trinidad na Tobago zimeona mabadiliko ya hivi majuzi yenye madhara na ya ubaguzi kwa sheria zao za uhalifu zinazolenga watu muhimu, na kuwasukuma mbali zaidi kutoka kwa matunzo na kuongeza hatari yao ya kupata VVU.

Tumaini lipo: Nchi na jamii zinaibuka kulinda mafanikio ya tiba ya VVU

Afrika Kusini kwa sasa inafadhili asilimia 77 ya mapambano yake dhidi ya UKIMWI, na katika mapitio ya bajeti ya 2025, imepanga kuongeza bajeti ya afya kwa asilimia 5.9 kila mwaka kwa kipindi cha miaka 3 ijayo, ikiwa ni pamoja na asilimia 3.3 ya ongezeko la mwaka kwa programu za VVU na kifua kikuu. Serikali pia inanuia kuanzisha mfumo wa taarifa za wagonjwa, mfumo wa usambazaji wa dawa za muda mrefu, na mfumo wa ufuatiliaji wa akiba ya dawa katika vituo vya afya.

Kufikia Desemba 2024, nchi 7 — Botswana, Eswatini, Lesotho, Namibia, Rwanda, Zambia, na Zimbabwe,  zilikuwa zimefikia malengo ya 95-95-95: asilimia 95 ya watu wanaoishi na HIV wanajua hali yao, asilimia 95 ya hao wapo kwenye matibabu, na asilimia 95 ya waliopo kwenye tiba wana kiwango kidogo cha virusi mwilini.

Ripoti pia inaangazia matumaini mapya kupitia zana za kisasa za kuzuia maambukizi kama vile PrEP ya sindano ya muda mrefu kama Lenacapavir, iliyothibitishwa kuwa na ufanisi mkubwa katika majaribio ya kitaalamu , ingawa changamoto za upatikanaji na bei bado ni kubwa.

Bado kuna nafasi ya kugeuza janga hili kuwa fursa. Nchi zinaongeza fedha za ndani. Jamii zinaonesha mbinu zinazofanya kazi. Sasa tunahitaji mshikamano wa kimataifa kuunga mkono ujasiri wao.” amesema Bi. Byanyima

Wito wa mshikamano

Ripoti ya UNAIDS ya 2025 inahitimisha kwa wito wa dharura. Mapambano dhidi ya VVU hayawezi kutegemea rasilimali za ndani pekee. Jumuiya ya kimataifa lazima ijitokeze kufidia pengo la ufadhili, kusaidia nchi kufikia malengo ya kinga na tiba, kuondoa vikwazo vya kisheria na kijamii, na kuziwezesha jamii kuongoza njia.

UNAIDS inasisitiza kwamba kila dola inayowekezwa katika kupambana na VVU si tu kwamba inaokoa maisha, bali pia inaimarisha mifumo ya afya na kuchangia malengo mapana ya maendeleo. Tangu mlipuko wa ugonjwa huu uanze, vifo 26.9 milioni vimeepushwa kupitia tiba, na watoto milioni 4.4 wamelindwa dhidi ya maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto.

Bi. Byanyima anasema,  “Katika wakati huu wa janga, ulimwengu lazima uchague mabadiliko badala ya kurudi nyuma. Kwa pamoja, bado tunaweza kukomesha UKIMWI kama tishio kwa afya ya umma ifikapo 2030, kama tutachukua hatua sasa, kwa mshikamano na dhamira thabiti bila kuyumbayumba."

0 Comment

UKIMWI:Mpango wa kutokomeza maambukizi ya vvu kwa watoto ifikapo 2030 wazinduliwa DRCAfyaclass Forum •

Wakati asilimia 91 ya watu wazima wa DRC wanaoishi na Virusi Vya Ukimwi, (VVU) wanapokea matibabu, ni asilimia 44 tu ya watoto wanaopata huduma hiyo – pengo lisilokubalika ambalo limekuwepo kwa zaidi ya muongo mmoja, na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imeazimia kulitatua.



Katika hatua ya aina yake ya kuziba pengo la muda mrefu katika matibabu dhidi ya Virusi Vya UKIMWI, VVU, Rais Félix Tshisekedi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC amezindua mpango wa kitaifa wa kutokomeza maambukizi ya UKIMWI kwa watoto nchini humo ifikapo mwaka 2030.

"Nchi yetu haiwezi tena kuvumilia watoto kuzaliwa na kukua na VVU wakati kuna zana za kuzuia, kugundua, na kutibu maambukizi haya kwa ufanisi," amesema Rais Tshisekedi wakati wa uzinduzi uliofanyika kwenye mkutano wa magavana huko Kolwezi, jimboni Lualaba.

"Kutokomeza UKIMWI kwa watoto ni wajibu wa maadili, hitaji la haki ya kijamii, na kiashiria cha heshima ya kibinadamu," ameongeza Rais Tshisekedi,  kwa mujibu wa ripoti ya shirika la Umoja wa Mataifa la kukabiliana na UKIMWI, UNAIDS.

UNAIDS inasema mpango huu mpya, unaoitwa IPESE (Initiative Présidentielle pour l’Élimination du Sida chez l’Enfant), ni ishara ya kujitolea upya kitaifa kuwafikia watoto ambao, licha ya mafanikio makubwa katika huduma za VVU kwa watu wazima, bado wameachwa nyuma kwa kiasi kikubwa.

Nchini DRC, maelfu ya watoto bado wanaambukizwa VVU kila mwaka kutokana na ukosefu wa upimaji kwa wanawake wajawazito, fursa iliyopotea ya kuokoa maisha ya akina mama na kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto.

Vipaumbele 4 muhimu

Mpango huu wa miaka mitano kutoka kwa Rais — ukiungwa mkono na ufadhili wa awali wa dola milioni 18 kutoka serikali ya kitaifa — unalenga kutoa mwitikio wa pamoja na wa kimkakati kupitia uongozi madhubuti wa kisiasa katika ngazi zote, ikiwemo magavana wa mikoa.

DRC imejizatiti kuharakisha maendeleo katika maeneo manne ya kipaumbele:

Kuboresha uchunguzi wa mapema na matibabu kwa watoto, vijana, na wanawake wajawazito

Kuzuia maambukizi mapya miongoni mwa watoto, vijana, na akina mama

Kuhakikisha matibabu ya haraka na ya moja kwa moja kwa wote waliogundulika kuwa na maambukizi

Kuondoa vikwazo vya kimfumo vinavyowazuia vijana kupata huduma za afya, kupitia njia zenye heshima, ushirikishwaji, na urafiki kwa vijana

Watoto wanaachwa nyuma

Wakati asilimia 91 ya watu wazima wanaoishi na VVU nchini DRC sasa wanapata matibabu ya kupunguza makali ya virusi (ARV), ni asilimia 44 tu ya watoto wanaoishi na VVU wanaopata huduma hizo — pengo ambalo limekuwepo kwa zaidi ya muongo mmoja.

Shukrani kwa ushirikiano kati ya serikali, jamii za kiraia, jumuiya za wenyeji, na washirika wa kimataifa kama PEPFAR, Mfuko wa Dunia, (Global Fund), UNAIDS, na Taasisi ya Elizabeth Glaser Pediatric AIDS Foundation, ufanisi wa matibabu kwa watu wazima umeongezeka kwa kasi. Lakini kwa watoto, mfumo bado unasuasua.

Kila mwaka, maelfu ya watoto wa DRC wanaambukizwa VVU, mara nyingi kwa sababu wanawake wajawazito hawachunguzwi — fursa iliyopotea ya kuokoa maisha ya mama na kuzuia maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto.

Hali hii inaonesha matatizo ya kimfumo: upatikanaji duni wa huduma bora za afya ya uzazi na jinsia kwa wanawake, ukosefu wa ujumuishaji mzuri wa huduma za VVU katika huduma ya afya ya mama na mtoto, minyororo dhaifu ya usambazaji wa dawa, na uratibu hafifu kati ya huduma za umma na jamii.

Huko Kolwezi, jimboni Lualaba nchini DRC, Rais Tshisekedi amesema kwamba DRC haitavumilia tena "watoto kuzaliwa na kukua wakiwa na VVU, ilhali kuna vifaa vya kuzuia, kugundua na kutibu maambukizi haya kwa ufanisi."

Tumaini jipya

UNAIDS imekaribisha mpango huu kama hatua muhimu inayohitajika sana wakati huu ambapo rasilimali za maendeleo ziko kwenye shinikizo kubwa.

"Katika kipindi ambapo ufadhili wa maendeleo unakabiliwa na changamoto na mifumo ya kusaidia walio hatarini zaidi imebanwa, uongozi wa Rais Félix Tshisekedi ni taa ya matumaini," amesema Dkt. Susan Kasedde, Mkurugenzi wa UNAIDS nchini DRC. “UNAIDS inaunga mkono kikamilifu mpango huu jasiri na wa kuhamasisha.”

Kupitia mpango huu, DRC inalenga kubadili mwelekeo wa kizazi kizima cha watoto ambao kwa muda mrefu wameachwa nyuma katika mapambano dhidi ya VVU.

"Tunatangaza ahadi ya kitaifa kuhakikisha kila mtoto wa Kongo ana haki ya kuzaliwa na kukua bila mzigo wa VVU," amesema Rais Tshisekedi. “Tuna njia za kufanikisha hili — na juu ya yote, tuna wajibu.”

TAGS: Afya/Afrika/DRC/VVU/PEPFAR/UNAIDS

0 Comment
Notification
My blog is in the process of editing and perfecting the new template, so there are still some functions to click but not yet used. Note which blogs associated with your side please read this lesson to update the blog logo.
UNDERSTOOD