Mlipuko wa Volkano Indonesia wasababisha Vifo na Watu Kupotea
Hofu imetanda katika jimbo la North Maluku nchini Indonesia baada ya mlipuko mkubwa wa volkano ya Mlima Dukono kusababisha vifo vya watu watatu na wengine zaidi ya 20 kutoweka.
Mlipuko huo ulitokea Ijumaa asubuhi wakati kundi la wapanda milima likiwa katika shughuli za utalii karibu na mlima huo maarufu wenye shughuli za mara kwa mara za volkeno. Mashuhuda walisema mlima ulianza kutoa mlio mkubwa kabla ya moshi mzito na majivu kusambaa angani kwa kasi.
Timu za uokoaji zilianza operesheni ya dharura mara baada ya tukio hilo, zikikabiliana na hali ngumu ya hewa pamoja na majivu yaliyofunika njia nyingi za kuelekea eneo la tukio. Serikali ya Indonesia imesema baadhi ya manusura wamefanikiwa kuhamishwa salama huku juhudi za kuwatafuta waliopotea zikiendelea.
Shirika la usimamizi wa majanga nchini humo limethibitisha kuwa watu watano wamejeruhiwa, wengi wao wakikumbwa na matatizo ya kupumua kutokana na moshi na majivu ya volkano.
Baada ya mlipuko huo, mamlaka zimefungia shughuli zote za wananchi na watalii ndani ya eneo la kilomita nne kuzunguka Mlima Dukono. Pia wananchi wameonywa kuwa mvua inaweza kusababisha mtiririko hatari wa matope ya volkano katika vijiji vya karibu.
Indonesia ni moja ya mataifa yenye volkano nyingi hai duniani kutokana na kuwa katika ukanda wa Pacific Ring of Fire, eneo linalokumbwa mara kwa mara na matetemeko ya ardhi pamoja na milipuko ya volkano.





Post a Comment
"Karibu kutoa maoni yako. Kumbuka: Link zote za matangazo haziruhusiwi na zitafutwa kiotomatiki".